Ajaribu Kujiua Kwasababu ya Kanumba, Kuburuzwa Mahakamani


BI. MARIAMU ELIUS [19] anatarajiwa kufikishwa Mahakamani muda wowote kuanzia sasa kwa kosa la kutaka kujiua kimakusudi akidai kifo cha Kanumba kimemgusa sana. Mariamu mkazi wa Kibaha Misugusugu alitaka kujiua mwanzoni mwa wiki hii kwa kile alichodai kuguswa na kifo cha msanii maarufu wa filamu nchini marehemu Steven Kanumba.

Mariam inadaiwa alitaka kujiua kwa kunywa sumu ya panya kwa kile alichokielezea mwenyewe kuwa ni masikitiko yake kutokana na kifo cha msanii huyo kwa kuwa alidai alimpenda sana akiwa katika tasnia hiyo ya kuigiza.

Taarifa ya kufikishwa mahakamani imetolewa na Jeshi la Polisi mkoani Pwani na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ernest Mangu.

Kamanda huyo amesema kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Jinai mtu akitaka kujiua ni kosa na watamfikisha mahakamani wakati wowote.

Mariamu amedaiwa kunywa sumu ya panya ili apoteze maisha kwa kile alichodai kumpoteza Kanumba kwa kuwa alisikitishwa na kuumizwa na kifo hicho.


Hata hivyo hakuweza kufanikiwa azma yake hiyo ya kujipeleka kuzimu na sasa yuko katika hospitali ya Tumbi Kibaha kwa matibabu akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi na atakapotoka na afya yake kuimarika atafikishwa mahakamani.