LULU AWAGOMEA MASTAA KUMUONA




STAA wa tasnia ya filamu Bongo ambaye kwa sasa yuko mahabusu Segerea akisubiri kusikilizwa kwa kesi yake inayomkabili, Elizabeth Michael ‘Lulu’, Aprili 14, mwaka huu aliwagomea mastaa wenzake kumuona walipokwenda kumtembelea lupango.

Chanzo chetu makini ambacho hakikauki gerezani hapo kila siku kilisema kuwa Lulu aliposikia kuna mastaa wenzake wa kike wamefika mahali hapo kumtembelea kwa ajili ya kumpa pole, aligoma kutoka nje huku akidai kuwa wengi wao wamekwenda ‘kumjoki’ tu.
“Alikataa katakata kutoka licha ya juhudi zote za kumbembeleza lakini hakuwa tayari kuonana nao,” kilidai chanzo hicho.
Kiliwataja baadhi ya mastaa waliokwenda gerezani hapo kumuona kuwa ni Sabrina Rupia ‘Cathy’ Halima Yahaya ‘Davina’ Mayasa Mrisho ‘Maya’ na wengineo.
Baada ya kupata taarifa hizo, paparazi wetu alimvutia waya Cathy ili kutaka kuthibitisha kama ni kweli waligomewa na Lulu ambapo alikiri ni kweli muigizaji mwenzao huyo kuwagomea.
“Ni kweli Lulu alitugomea kabisa kumuona, alituma ujumbe kuwa anayestahili kwenda mahali hapo kumuona ni mama, shangazi na mama yake mdogo tu, hao ndiyo amewapendekeza kwenda kumuona lakini hakuna staa hata moja mmoja ambaye yuko tayari kuonana naye,” alisema Cathy.