SIJAOMBA FEDHA ZAIDI - RONALDO.
MSHAMBULIAJI nyota wa
kimataifa wa Ureno na klabu ya Real Madrid ya Hispania Cristiano Ronaldo
amesema kuwa kukosa kwake furaha katika klabu hiyo hakuhusiani na mambo
ya fedha kama baadhi ya vyombo vya habari vinavyosema kwani kikubwa
anachotaka yeye ni mkataba wenye faida zaidi. Mshambuliaji huyo ghali
zaidi duniani alitawala vyombo vya habari baada ya ushindi wa timu yake
wa mabao 3-0 dhidi ya Granada Jumapili iliyopita wakati alipokataa
kushangilia mabao mawili aliyofunga katika mchezo huo na baadae kusema
kuwa alikuwa na huzuni. Ronaldo aliandika ujumbe katika ukurasa wake
kwenye mtandao wa kijamii wa twitter kuwa kuonyesha uzuni aliyokuwa nayo
kumezua mjadala mkubwa huku watu wakimtuhumu kuwa anahitaji pesa zaidi
lakini siku moja watu hao watakuja kuona kwamba huzuni yake haihusiana
na suala la kuongezwa fedha. Kuna taarifa pia zilizochapishwa na vyombo
vya habari nchini humo kuwa mchezaji huyo alifanya mkutano na rais wa
klabu hiyo Florentino Perez Jumamosi na kumwambia kuwa hadhani kama
anapewa ushirikiano katika vyumba vya kubadilishia nguo, hana furaha na
anataka kuondoka klabuni hapo. Ronaldo ambaye ni mojawapo ya wachezaji
wanaolipwa zaidi duniani akikinga kiasi cha dola milioni 13 kwa mwaka,
alikana tetesi zote hizo na kuwahakikishia mashabiki wa Madrid kwamba
bado ana nia ya kubakia hapo na kushinda mataji zaidi.