Mahudhurio Ya Wajumbe Yamkatisha Tamaa Dk Slaa


 KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeeo( Chadema), Dk Willbrod Slaa jana alizungumzia kukatishwa kwake tamaa na mahudhurio ya wajumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho Jimbo la Kinondoni jijini Dar es Salaam.Dk Slaa alisema hayo jana wakati wa Mkutano Mkuu wa jimbo hilo baada ya mahudhurio kuwa hafifu. 

Alisema asilimia 50 ya mahudhurio ya wajumbe katika jimbo hilo ni aibu na yanatia shaka iwapo wana nia ya dhati ya kushika dola mwaka 2015.“Dalili hii inaonyesha kwamba kuna tatizo, hivyo kupitia mkutano huu tutayamaliza na kurudisha ufanisi wa chama” alisema Dk Slaa na kuongeza:
“Chadema ni chama ambacho kinajiandaa kushika dola mwaka 2015, endapo hali hii itaendelea ya wajumbe kutafutana kwa njia ya simu itakuwa hatari wakati wa kuunda baraza la mawaziri” alisema na kuongeza:
“Haiwezekani Rais akawa anatafuta baraza la mawaziri kwa njia ya simu, kwani bila kujipanga wakati huu itakuwa ngumu huko mbele tunakokwenda,” alisema.Katika mazungumzo yake Dk Slaa alisema, wanakusudia kutoa tamko la nini ifanyike kuhusu mauaji mbalimbali ya wananchi yalifanywa na polisi baada ya Rais Jakaya Kikwete kushindwa kuwachukulia hatua Waziri wa Mambo ya Ndani , Dk Emmanuel Nchimbi, Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Saidi Mwema na Kamanda wa Mkoa wa Iringa Michael Kamhanda. 
“Hatuwezi kutulia huku tukiona vyombo ambavyo vinatakiwa kulinda usalama wa raia ndio vinakuwa vya kwanza kuwaua raia wasiokuwa na hatia huku kiongozi wa nchini (Rais Kikwete) akiwa kimya bila kutoa tamko lolote,” alisema.
Katika mkutano huo, wajumbe walitakiwa kufika mapema kwa ajili ya kuanza kwa mkutano saa 4 hadi saa 6 mchana, lakini kutokana na ufinyu wa mahudhurio, mkutano huo ulianza saa 6.47 mchana.
Sifa zimwendee Mwenyekiti wa Chama hicho Jimbo la Kinondoni, Deo Mushi ambaye alifanya kazi ya kuwatafuta wajumbe hao kwa njia ya simu ili kutimiza idadi ya asilimia 50.
Mratibu wa Mkutano huo, Mkurungenzi wa Sera na Utafiti wa Chama hicho, Chacha Mwita, alisema wajumbe waliokuwa wamefika walikuwa hawana uwezo wa kuruhusu kufanyika kwa mkutano huo.
Mwita alisema idadi ambayo inatakiwa ya wajumbe wote ni zaidi ya 120, lakini waliokuwa wamefika walikuwa hawazidi 50.
Soma zaidi: http://www.mwananchi.co.tz