Mastaa wa filamu wamtenga Lulu



KITENDO cha mastaa wa filamu kushindwa kwenda kumtembelea msanii mwenzao, Elizabeth Michael ‘Lulu’, anayekabiliwa na kesi inayohusisha kifo cha aliyekuwa mwigizaji, Steven Kanumba, katika gereza la Segerea jijini Dar ni kukwepa kuhusishwa katika keshi hiyo, imefahamika.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa kumekuwa na mahudhurio hafifu ya wasanii maarufu kwenda kumtembelea Lulu katika gereza hilo.
Akielezea hali hiyo, kiongozi mmoja wa Bongo Movie, alisema ni kweli hali hiyo ipo na wengi wanaogopa kuhusishwa katika kesi hiyo kwa kuwa bado uchunguzi wake unaendelea.
“Napingana na hoja ya kusema sisi mastaa ni wanafiki, binafsi ninachokiogopa mimi na wenzangu ni majumba mabovu ambayo yanaendelea kubomoka (kuingizwa kwenye tuhuma) kila siku kuhusiana na kesi ya Lulu, ndiyo maana wengi wanaogopa kwenda Segerea,” alisema kiongozi huyo.
Lulu ambaye anatuhumiwa kuhusika na kifo cha Kanumba, ameshapandishwa kizimbani mara moja na atarejea tena Aprili 23, mwaka huu.
Kanumba alifariki dunia usiku wa kuamkia Aprili 7, mwaka huu, nyumbani kwake Sinza Vatican, Dar na kuzikwa Aprili 10 katika makaburi ya Kinondoni.