SAKATA LA USAJILI WA NGASSA - SIMBA WATUMA OFA YA MIL.25, YANGA MIL.20: NGASSA ASEMA ATACHEZA POPOTE ATAKAPORIDHIKA NAPO

Siku moja baada ya klabu ya Azam kutangaza kumuweka sokoni Mrisho Khalfan Ngassa kwa ada ya uhamisho wa $50,000, kulwa na doto wa soka la Tanzania vilabu vikongwe Simba na Yanga vimetuma ofa rasmi ya kutaka kumsaini mshambuliaji ambaye pia anaichezea timu ya taifa ya Tanzania.Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na klabu ya Azam kupitia mtandao wake rasmi hadi sasa klabu ya Simba imetuma ofa ya shilingi millioni 25 na Yanga wametuma millioni 20.

Taarifa hiyo ilisomeka: "Hadi hivi sasa Ofa ya Simba ni shilingi Milioni 25 na Yanga ni Milioni 20. kutokana na hilo. Simba wapo kwenye nafasi kubwa ya kumnyakua Mrisho Ngasa. Kesho ni siku ya Mwisho. Ingawa tungependa kumuuza Mrisho Ngasa Yanga lakini tutampeleka kwa timu iliyotoa ofa nzuri zaidi


Lengo la Azam FC lilikuwa ni kumpeleka Mrisho kwenye timu ambayo atacheza kwa raha na amani, kutokana na yeye kuivaa na kuibusu Jezi ya Yanga siku ambayo Azam FC haikuwa na mchezo na Yanga... 


Azam FC inaamini kuwa Yanga ilikuwa Sehemu sahihi kwa Mrisho, lakini uongozi wa Yanga umeonekana kutokuwa na haja na Mrisho na ndiyo maana umeonekana kukataa kutoa ofa ya maana. Kutokana na sababu hizo Azam FC italazimika kumuuza Mrisho Ngasa Simba kwani hatuhitaji kuwa na mchezaji ambaye anafanya vitendo vya kuidharau brand ya Azam FC ambayo tunajaribu kuijenga."


Baada ya kutoka kwa taarifa tuliwasiliana na mchezaji mwenyewe Mrisho Ngassa kuzungumzia suala la uhamisho wake alisema: "Mimi nina mkataba na Azam na wao ndio wana maamuzi dhidi yangu. Kama wameamua kuniuza mie sina tatizo. I am proffesional footballer, hii ndio kazi yangu na nitaifanya popote nitakaporidhika napo."