
Na: Mwandishi 
wa Thehabari.com
SEKRETARIETI 
mpya ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyoingia madarakani hivi karibuni chini ya 
uongozi wa Rais Jakaya Kikwete, imesema itahakikisha vitendo vya rushwa hasa 
kwenye chaguzi za chama hicho vinakoma mara moja, tofauti na ilivyokuwa 
imezoeleka. 
Kauli hiyo 
ya viongozi wa juu wa CCM, Mwenyekiti Taifa (Rais Kikwete), Makamu Mwenyekiti 
Tanzania Bara (Phillip Mangula) na Katibu Mkuu (Abdulrahman Kinana) imetolewa 
jana na viongozi hao wakati wakizungumza na wana-CCM Mkoa wa Dar es Salaam 
katika mkutano wa kumpongeza Rais Kikwete kuchaguliwa kushika nafasi hiyo 
tena.
Akizungumza 
na umati wa wanachama hao, Rais Kikwete aliwataka viongozi wapya kufanya kazi ya 
ziada ya kuhakikisha wanarejesha imani ya Watanzania kwa CCM, ambayo haiko kama 
ilivyokuwa zamani. 
“Lazima 
kujiuliza nini kimekifanya chama hiki kufikia hapo kilipo na kuangalia nini cha 
kufanya ili kuondokana na hali hiyo. Pale mnapohisi hali ya kuungwa mkono 
inapungua lazima tujiulize, kulikoni..! Nini cha kufanya ili kuimarisha chama,” 
alisema na kuongeza kuwa kazi nyingine ni kuhakikisha wanakijenga chama na 
kuimarisha zaidi ili kiendelee kuwaongoza Watanzania.
“Chama chetu 
hakifanyi mikutano…wenzetu wanafanya kwanini sisi hatufanyi, sasa tutatengeneza 
utaratibu maalumu kuhakikisha viongozi wa chama kwa nafasi zao wanafanya kazi 
yao ipasavyo ndani na nje ya chama,” alisema Rais Kikwete.
Alisema ipo 
haja ya kujipanga na kuangalia namna ya kupambana na propaganda hasi za baadhi 
ya vyombo vya habari na wapinzani ili kukabiliana na hali hiyo. Aliwataka 
wanaCCM kuacha makundi na chuki ambayo yamekuwa yakikigawa chama hicho. 
Awali 
akizungumza Kinana alisema vitendo vya rushwa ndani ya CCM watahakikisha 
vinakoma mara moja ili kurejesha imani ya Watanzania iliyopungua kutokana na 
tuhuma za wachache dhidi ya vitendo viovu.
Alisema 
chini ya uongozi wake atahakikisha mashaka yaliotawala kwa wananchi dhidi ya CCM 
yanaondoka kwa kuwaengua wale wanaoendeleza vitendo vya rushwa, majumbu na 
vitendo vinavyo leta sifa mbaya ya chama hicho.
“Hatuwezi 
kuiongoza nchi yetu wakati watu wanamashaka na sisi, lazima tuondoe mashaka 
akisimama mwana-CCM wote waseme naam huyu anaweza kusema…sio akisimama mwana-CCM 
kusema watu wanahoji haaah, na huyu naye anakemea rushwa? 
Aliwataka 
wana-CCM kushirikiana katika kukisafisha chama na si kuwaachia viongozi jukumu 
hilo, ambalo wao kama viongozi wamekubali kuongoza mapambano hayo.
Alisema CCM 
ina wanachama milioni 5 ambao asilimia 99.9 wengi wakiwa ni masikini na 
waadilifu huku asilimia 0.1 wakiwa ni wala rushwa wakubwa, wapenda mizengwe, 
wapendeleaji hivyo kujikuta idadi hiyo ikikichafua chama chote jambo ambalo 
alisema chini ya uongozi wao hawawezi kuacha hali hiyo iendelee.
Alisema 
atahakikisha anasimamia ilani ya chama vizuri huku kanuni mbalimbali zikifuatwa 
ili kuleta haki ndani ya chama hicho, alisema kuna kazi kubwa ya kukijenga chama 
hicho,
Alisema 
pamoja na viongozi wenzake watahakikisha baadhi ya wana-CCM waliokuwa na tabia 
za mizengwe pamoja na kupanga safu za viongoli ili kubebana kimaslahi inatoweka, 
hivyo kumtaka kila mwanachama afanye kazi ya kumuingizia kipato na si kutegemea 
kunufaika na nafasi ya uongozi.
Naye Makamu 
Mwenyekiti Bara, Mangula alisema wapo baadhi ya viongozi wameingia ndani ya 
chama kwa rushwa na tayari malalamiko juu ya mizengwe ya uchaguzi wa chama hicho 
uliofanyika yamewafikia, hivyo kwa sasa wataanza kupitia kwa kina kila 
malalamiko na atayebainika kuingia kwa rushwa ataenguliwa bila kumuogopa. 
“Tunajipa 
miezi sita ndani ya miezi sita walioingia kihalali wataendelea lakini walioingia 
hovyo hovyo ‘out’…walioingia kwa pesa nje, hata wale waliokuwa wanatumwa 
vibahasha nao tukiwajua wale nje, hatukubali chama chetu kituhumiwe kwa rushwa, 
wala hatuta ngoja ushahidi sijui wa TAKUKURU, Polisi hakuna tutakisafisha Chama 
Cha Mapinduzi,” alisema.
“…Lakini na 
nyingi mliokubali kununuliwa kama sambusa mlifanya makosa, tusikubali 
tena…kwanini mtu ukubali kuthaminishwa kama sambusa?,”
 
