Ilianza ishara moja ambayo wengi waliidharau lakini werevu walioamua kuichambua na kulinganisha na matukio walibaini kitu. Wiki chache zilizopita, status ya Facebook ya Diamond ilibadilika kutoka ‘single’ hadi ‘in a relationship’.
Baada ya siku tangu kubadilika kwa status hiyo, video ya Leka Dutigite ilitoka na kupigia mstari mashaka ya wengi kuhusiana na kama wapenzi hao wa zamani wamerudiana tena.
Katika video hiyo Diamond na Wema walionekana wakiwa wamekaa karibu na kuonesha dalili zote kuwa mapenzi yao yamerudi kwa kasi.
Wema
anaonekana kwenye video hiyo akiwa kama ‘the most happiest chick on
earth’ kwa kumshika Diamond mkono wake na kufurahia safari ya boti
ndani ya ziwa Tanganyika wakati wa uchukuaji wa video hiyo ya Kigoma
All Stars.
Wema aliamua kumsindikiza mpenzi wake huyo kwakuwa hakutaka kumwacha mpweke ugenini mkoani Kigoma.
Baada ya muda kidogo Diamond akaugua ghafla na kuonekana akiwa kwenye kitanda cha hospitali na daktari akimhudumia.
Picha hizo zilisambaa kwenye internet na kuzua maswali mengi nini kimemsibu kijana huyo. Lakini baadaye tena ikatokea picha nyingine ya Wema Sepetu akiwa kwenye kitanda hicho hicho alichokuwa Diamond.
Hitimisho la walioziona picha hizo ni kuwa hiyo ni hospitali iliyozoeleka kutumiwa na wapenzi hao na huenda daktari anayewatibu ni mmoja kwakuwa ndiye anayeonekana kwenye picha zao zote.
Matukio hayo yanatoa majibu ya asilimia 100 kuwa mastaa hawa wamerudiana tena.
Hata hivyo hakuna sehemu waliyokiri kuwa wamerudiana licha ya dalili zote hizo kuonekana.
“Kama kuna watu watatuona leo, wasifikiri kwamba ni wapenzi ila kirafiki tu. Ndani ya moyo wangu kwa sasa simchukii tena Diamond, naamini hata yeye ni hivyohivyo.”
Hata hivyo hii si mara ya kwanza kurudiana baada ya kuachana. Wamewahi kuachana mwaka jana tena na kurudiana kwa kasi mpaka kuvalishana pete.
Kuachana kwao kwa mara ya mwisho kulikuwa na mshindo mkubwa kuliko ilivyokuwa mwanzo. Miongoni mwa watu waliochangia kuachana kwao ni pamoja na Jokate Mwegelo aliyeingia ndani ya picha hiyo. Jokate na Diamond wamekuwa na uhusiano mfupi wa chinichini ambao Diamond mwenyewe aliuthibitisha. Haijulikani hata hivyo wameachana vipi!!
Ukaribu wa Jokate na Diamond uliongezeka kutokana na video ya Mawazo ambayo ilizua ugomvi mkubwa kati ya Wema na Diamond na kuchochea zaidi kuachana kwao. Tuna mashaka kama warembo hao wanasaliamiana tena ama kama beef lao limeisha.
Mwezi April mwaka huu ugomvi wa Diamond na Wema ulifika level nyingine mbaya zaidi kiasi cha wapenzi hao kuanika mambo mazito juu yao kwenye radio.
Diamond alikiri kuachana na Wema mwezi January mwaka huu na hiyo ni kutokana na kukerwa na tabia za Wema alizozikemea lakini mwisho wa siku hakufanikiwa.
Wema alidaiwa kuwalipa waandishi wa habari wa magazeti ili watoe stori zake na Diamond alikua anawalipa waandishi wasiandike chochote.
Beef lao lilifikia pabaya pia kwenye show ya Diamonds Are Forever ya Mlimani City mwishoni mwa mwezi March ambapo Diamond alikataa kupokea pesa kwa Wema Sepetu aliyokua anampa kwenye stage kwa sababu ya kukwepa mambo yake.
Kitendo hicho kilimtoa machozi Wema Sepetu na hivyo kukuza zaidi drama inayozunguka uhusiano wao.
Na sasa kwakuwa kila dalili zinaonesha kurudi kwa mahaba kati yao, swali ni Je! How long can they go?