KIONGOZI WA NIDHAMU BONGO MOVIE AJITOA


MWIGIZAJI mahiri katika tasnia ya filamu Bongo Herieth Chumila aliyekuwa ni kiongozi wa nidhamu katika kundi la Bongo Movie Unity linaloundwa na wasanii wenye majina ameachia ngazi.
"Ni kweli nimejitoa katika uongozi wa kundi hilo kutokana na matukio yanayotokea katika kundi hilo la Bongo Movie ya utovu wa nidhamu katika jamii yetu.
 
  Sisi ni watu tunaojiheshimu katika familia zetu, inakuwa vigumu jamii kutuelewa kama nasi si kati yao ya wasanii hao wenye kashifa, jambo la msingi ni kujiudhuru katika uongozi," alisema Herieth.

Msanii huyo amebainisha kuwa hali ya kundi hilo kwa sasa si kama zamani limegawanyika na kukosa muda wa kukutana na kuweza kuonyana hata kupeana ushauri kama ilivyokuwa awali jambo lilomfanya mwanadada huyo kumwaga manyanga katika uongozi huo kama kiongozi wa nidhamu katika kundi hilo na sababu kuu kuogopa kutukanwa na wasanii hao waliojipindia.

Herieth alifikia uamuzi huo baada wasanii wawili wa kundi hilo Wema Sepetu na Aunty Ezekiel kukumbwa na kashfa ya kucheza katika majukwaa nusu uchi hivi karibuni huku baadhi ya wasanii wa kundi pia kuvuma kwa kashfa za ngono.