Mtaalamu Adai Kuna Mashine,Vipimo Feki Vya Ukimwi Nchini



Na:  Florence Majani -Mwananchi.


WAKATI joto la kusambaa kwa dawa bandia za kupunguza makali ya Ukimwi (ARV), likiwa bado halijapoa, Mkemia Mkuu Mstaafu wa Serikali, Dk Juma Madati amedai kuwa ripoti yake inayoeleza kuhusu kuwapo kwa vipimo bandia vya kupimia Ukimwi imewekwa kapuni.Dk Madati aliliambia Mwananchi Jumapili hivi karibuni katika mahojiano maalumu kuwa ripoti yake ya mwaka 2007 aliyoiwasilisha serikalini kuhusu kuwapo kwa vipimo feki vya kupima Virusi vya Ukimwi (VVU) na mashine za kupima kiwango cha CD4 mwilini haijafanyiwa kazi wala kufanywa ufuatiliaji.

Mkemia mkuu mstaafu huyo, ambaye ni mmoja wa wajumbe wa tume iliyoundwa na aliyekuwa Waziri wa Afya wakati huo, Profesa David Mwakyusa mwaka 2007 kuchunguza sakata la kuingizwa nchini kwa vipimo feki vya kupima VVU na mashine za CD4, alidai kuwa waziri huyo hakutumia ripoti sahihi iliyoeleza ukweli na uwazi kuhusu mashine na vipimo hivyo.

Alisema kwamba Profesa Mwakyusa alitumia ripoti za wajumbe wawili pekee wa tume hiyo, aliowataja kuwa ni Profesa Philip Hiza ambaye ni Mganga Mkuu Mstaafu na Profesa Raphael Lema, Mtafiti Mkuu wa Magonjwa wa Serikali, ambaye kwa sasa ni marehemu.

Dk Madata alidai kuwa ripoti za wenzake hao ambazo zilitumiwa na Serikali hazikuweka wazi ukweli kuhusu vipimo vyote vinavyotumika kupima VVU na mashine za CD4.

Hata hivyo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi alipoulizwa jana kuhusu taarifa hiyo alisema hajawahi kuiona ripoti hiyo ya Dk Madati na kuahidi kuwa, ataitafuta kupitia watendaji wa wizara yake na pia atawasiliana na mtafiti huyo ili kujua undani wa suala hilo na kuchukua hatua za haraka.
Alisema kuwa kwa nafasi yake ya msimamizi mkuu wa kuhakikisha usalama wa afya za Watanzania hawezi kuliachia suala hilo lipite hivihivi, bali atalifuatilia hadi ukweli utakapofahamika.
"Kwa kweli sina taarifa kuhusu kuwapo kwa ripoti hiyo ya uchunguzi, lakini nitawasiliana na watendaji wangu wizarani ili niweze kuiona…: Nitatafuta fursa pia ya kuonana naye (Dk Madati), ili anifafanulie kwa undani juu ya ripoti yake,” alisema Dk Mwinyi.
Alipoulizwa kuhusu sakata hilo, Profesa Mwakyusa ambaye alikuwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii wakati ripoti ya Dk Madati ilipowasilishwa serikalini, alikiri kuwa aliunda kamati ya wataalamu watatu kuchunguza jambo hilo akiwamo, Dk Madati.
Alisema kuwa, tume hiyo ilifanya kazi yake na kumkabidhi ripoti, lakini hakumbuki kama Dk Madati hakushirikishwa.
Profesa Mwakyusa alieleza kama Dk Madati hakushirikishwa alitakiwa kutoa  taarifa wakati huo, badala ya kulalamika sasa.
“Sijui kama Madati hakushirikishwa na kama alipata matatizo hayo, basi angenitaarifu wakati huo,” alisema Profesa Mwakyusa.

Ripoti ya Dk Madati
Dk Madati alisema ripoti ya timu yake ilibaini kuwa vipimo na mashine hizo, zinazojulikana kama Capillus na Cyflow CD4, hazina ubora hivyo kulikuwa na uwezekano wa mtu kupima na kupewa majibu yasiyo sahihi.

Alifafanua kuwa kutoshirikishwa kwa ripoti yake kunaonyesha kuwa rushwa ilitawala kwa kiasi kikubwa katika uingizwaji na usambazwaji wa mashine hizo na vitendanishi vyake.

“Niliandika ripoti iliyoonyesha kuwa vifaa vilivyotoka Kampuni ya … (jina tunalihifadhi) ya nchini Marekani, havikuwa na ubora na kuwa Wizara ya Afya ilifanya uzembe tangu wakati wa ununuzi. Lakini, ripoti yangu haikutumika, badala yake zilitumika za wenzangu wawili, ambao hawakunipa ushirikiano wakati wa uchunguzi wetu,” alisema Dk Madati.

Aliongeza; "Majibu ya wenzangu yalionyesha kuwa mashine kutoka Ujerumani ndizo zilikuwa feki wakati si kweli."

Daktari huyo aliyezungumza na gazeti hili akiwa nyumbani kwake, alisema kuwa alipomaliza kazi yake aliipeleka ripoti hiyo kwa waziri, ambaye alimpa sifa kwa kazi nzuri, lakini jambo la kushangaza waziri huyo hakuzitumia taarifa za ripoti yake, wala kumwita katika kikao cha waandishi wa habari kama alivyowaita wenzake wawili.

“Nina wasiwasi mkubwa kuwa hata sasa, bado watu wanapata majibu yasiyo sahihi kwa sababu wanatumia vitendanishi kutoka Marekani ambavyo siyo bora,” alisema.

Ripoti ya Profesa Lema na Profesa Hiza, zilionyesha kuwa vifaa vilivyosambazwa na Kampuni ya Partec kutoka Ujerumani, ndivyo vilivyokuwa na upungufu.

Ripoti hiyo ilionyesha kuwa mzabuni aliyeleta mashine hizo nchini hakuwa mtaalamu wa kutengeneza mashine hizo, zaidi ya kuwa mshauri wa Kampuni ya Partec Essential Health Care na kwamba wizara haikuhusika na ucheleweshaji vitendanishi hivyo, jambo lililodaiwa kusababisha mashine hizo kutoa majibu yasiyo kweli.

Dk Madati alisema kuwa majibu ya tume yaliyotolewa na Profesa Mwakyusa ni ya watu wawili pekee, wakati ripoti yake iliyoachwa ilionyesha matokeo ya kina zaidi ya hayo.

Majibu ya tume hiyo ya watu wawili, yalisababisha kupigwa marufuku kwa mashine za Cyflow, badala yake mashine za FACSCount kutoka Marekani zikaanza kutumika.
Baada ya hatua hiyo, Kampuni ya Partec ililalamikia kuhujumiwa na Wizara ya Afya wakati huo, kwa sababu mbalimbali ikiwamo rushwa.
Katika ukurasa wa saba, ripoti ya Dk Madati inaonyesha kuwa kampuni nyingine ambayo nayo jina lake tunalihifadhi, iliombwa rushwa na watu kutoka Wizara ya Afya, ili kuzifanyia uchunguzi mapema mashine hizo.
Dk Madati alisema ripoti yake ilionyesha kuwa, Serikali ilianza kukosea tangu awali katika ununuzi wa vitendanishi.
Dk Madata alidai;  “Nina hakika watu wengi walikufa kwa sababu ya kupata majibu yasiyo sahihi, kwani hakuna mtaalamu wa afya asiyejua kuwa dawa zinazotumika katika mashine hizo, hazifanyi kazi katika joto kama la hapa Dar es Salaam. Walilifahamu hilo, lakini rushwa ilisababisha Serikali kununua vitendanishi hivyo.”

Alisema  ripoti yake ilibainisha kuwa, Wizara ya Afya ilinunua mashine za kupimia CD4, ambazo hazitambuliki na Shirika la Afya Duniani (WHO).
“Mashine za CD4 kutoka Marekani zilikuwa kubwa pengine zinaweza kujaa hata chumba kimoja kikubwa, halafu hazikuwa na uwezo wa kupima watu wengi, kutokana na mchakato wake mrefu wa kupima.  Kwa mfano hospitali yenye wagonjwa 200, watapimwa wagonjwa 10 au 15 tu kwa siku," alisema.
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa mashine za Ujerumani zilizoitwa CD4 Cyflow machine zilikuwa rahisi kutumia na hazikuwapa shida  wataalamu wa afya.