Mbunge Wa CCM Alivyo Timuliwa Bungeni


Neville Meena, Dodoma
NAIBU Spika wa Bunge, Job Ndugai amemwadhibu Mbunge wa Kigamboni (CCM), Dk Faustine Ndungulile kutohudhuria vikao vitatu mfululizo baada ya kushindwa kuthibitisha tuhuma kwamba madiwani wa Halmashauri ya Manispaa Temeke walihongwa ili kuukubali Mradi wa Mji Mpya wa Kigamboni.Ndugai alitumia kifungu cha 73 (3) ambacho kinampa mamlaka ya kumwadhibu mbunge aliyeshindwa kuthibitisha tuhuma alizozitoa, huku pia akiwa amekaidi kufuta kauli yake kuhusiana na tuhuma hizo.

“Kwa kutumia kifungu namba 73 cha Kanuni za Bunge, hutahudhuria vikao vya Bunge mara tatu mfululizo, askari mtoeni nje,” aliagiza Ndugai.

Awali, Dk Ndungulile alishtakiwa na madiwani wanne wa Kigamboni kwamba aliwatuhumu kupewa rushwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, ili waunge mkono mradi wa kuendeleza mji huo mpya wa Kigamboni.