DIEGO MARADONA: NILIGUNDUA KUTIMULIWA KWANGU KUPITIA TWITTER

Baada ya jaribio lake la kutaka kuendelea na kibarua chake kwenye timu ya Al Wasl, Diego Maradona ametoa kali nyingine baada ya kusema aligundua ametimuliwa kwenye klabu hiyo kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter.Maradona, 51, alitimuliwa na Al Wasl mapema mwezi huu baada ya kuwa na msimu mbaya wa kwanza kwenye mkataba wake wa miaka miwili aliosaini mwezi May 2011.

Sasa baada ya wiki iliyopita kukataa uamuzi wa kutimuliwa na kusisitiza atakutana na viongozi wa timu hiyo ya Dubai na kumaliza tofauti zao zilizopelekea kutimuliwa, leo hii maradona ameibuka na kuiambia radio station ya Perros de la Calle kwamba hakutaarifiwa rasmi uamuzi wa kutimuliwa mpaka pale alipokuja kugundua kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter.

"Ukweli ni kwamba niligundua kuota nyasi kibarua changu kupitia Twitter sio jambo zuri. Nilikuwa nafanya kazi mpaka pale walipoamua kufanya mabadiliko. Klabu ni mali yao na siwezi kusema chochote kwa kuwa wao ndio wana haki  ya kufanya chochote pamoja na kuchagua kocha wao."

Mpaka wiki iliyop[ita Maradona hakuwa amepokea taarifa rasmi ya klabu ya kumtimua kazi, mpaka pale mwenyekiti wa Al Wasl Mohamed Bin Dukhan waliwasiliana na Maradona kupitia ubalozi wa Argentina kwa msaada wa mtafsiri lugha wa kihispaniola.