
Na: Kelvin Matandiko- Mwananchi.
JESHI
 la Polisi kupitia kikosi cha Usalama barabarani  nchini kimesema  jumla
 ya ajali za pikipiki (bodaboda) 2601 zilizotokea kuanzia Januari hadi 
Juni mwaka huu zilisababisha vifo vya madereva  487 wa pikipiki hizo.
Akizungumza
 na gazeti hili jana ofisini kwake, Kamishna Msaidi wa Polisi, kikosi 
cha usalama barabarani Johansen Kahatano alisema ajali hizo zinazidi 
kuongezeka kila mwaka kutokana na sababu mbalimbali.
“Kwa
 mwaka 2009 kulitokea ajali 3406 na waliokufa ni 502,mwaka uliofuata 
ajali 4363 na vifo 683 na ilipofikia mwaka 2011 zilitpkea ajali zingine 
5384 na waliokufa ni 945, taarifa hii inaonyesha kuwa kila mwaka vifo 
vinaongezeka”alisema Kahatano.
Alisema
 kuongezeka kwa bodaboda na uelewa mdogo wa sheria za usalama barabarani
 kwa madereva hao ndiyo  sababu kubwa ya ongezeko la ajali hizo.
Alisema
 pikipiki zilizo sajiliwa mwaka 2009 kwa ajili ya biashara hiyo ni 
87,826 na hadi kufikia mwaka 2011 kulikuwa na pikipiki  1,34,831 na 
kwamba wamiliki wake  wamekuwa hawana elimu ya kutosha kwa ajili ya 
kuwasaidia madereva wao.
Aliongeza
 kuwa kutokana na changamoto hiyo wamepata msaada kutoka kwa Taasisi 
zisizo za kiserikali kwa mikoa mbalimbali hapa nchini zinazotoa elimu ya
 mafunzo ya udereva kwa pikipiki ili kupunguza ongezeko la ajali
“Mafunzo
 hayo yalianza Juni mwaka huu,Kwa mkoa wa Tanga kuna taasisi  inayoitwa 
APEC inatoa mafunzo kwa Bodaboda 2000 hadi sasa na Mkoa wa Mtwara 
inaitwa British Gas inatoa mafunzo kwa Bodaboda 600,lengo ni kupunguza 
ajali hizi kote nchini”alisema Kahatano.
Hata
 hivyo alikiri kuelemewa na utekelezaji wa jukumu la kukamata waendesha 
pikipiki  wanaovunja sheria barabarani kutokana na wingi wao 
ukilinganisha na uchache wa Askari wa usalama barabarani.
Kwa
 sasa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Sumatra limeingia makubaliano 
na halmashauri zote nchini kuanzia Julai mwaka huu kutoa leseni ya 
biashara kwa kila dereva wa bodaboda ili kuwatambua rasmi na kupunguza 
matukio ya ukabaji dhidi yao.
Aidha
 aliwataka madereva wote na wamiliki wao kutambua sheria za barabarani 
na kujali uhai wao pindi wanapokuwa barabarani  na kwamba endapo kila 
mmoja atafanya hivyo itakuwa ni njia sahihi ya kupunguza au kumalizika 
ajali hizo.